MAKABIDHIANO YA MADAWA NA VIFAA TIBA YAFANYIKA ZANZIBAR

Waziri wa Afya Ustawi wa Jamii Wazee Jinsia na Watoto (kulia)akipokea Msaada wa Madawa kutoka kwa Muakilishi wa shirika la GLOBAL LIFE SHARING Hyeksu Kim (kushoto)katika hafla ya makabidhiano iliofanyika katika Ukumbi wa Bohari kuu ya Madawa Maruhubi Zanzibar.

Wizara ya Afya Zanzibar imepokea msaada wa vifaa tiba na dawa mbalimbali kutoka Shirika la Global Life Sharing la Korea ya Kaskazini.

Akipokea msaada huo huko Bohari kuu ya Dawa Maruhubi, Waziri wa Afya Ustawi wa Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto, Nassor Ahmed Mazrui amesema msaada huo umekuja wakati muafaka  kwa vile Serikali inahitaji dawa hizo.

Waziri huyo, amesema atahakikisha msaada huo unatumika kama ilivyokusudiwa  na kusambazwa katika vituo vyote vya Unguja na Pemba ili kuhakikisha wananchi wanapata matibabu yalio bora.

Sambamba na hilo, Waziri Mazrui ametoa onyokali kwa wafanyakazi wa Wizara hiyo na wauza madawa ambao watabainika kuuza dawa kinyume na utaratibu ambazo zinatolewa na Serikali na hatua kali kuchukuliwa dhidi yao, ikiwemo kufutiwa leseni pamoja na kufukuzwa kazi kwa mtumishi yoyote anaehusika na kadhia hiyo.

Kwa upande wake mwakilishi kutoka Shirika la Global life Sharering, Hyeksu Kim, amesema ataendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutoa misaada kwa kipindi cha miaka mitano ili kupunguza changamoto ya dawa ambayo imekuwa ni kikwazo kwa wananchi.

Aidha amesema lengo lao ni kuona afya za wananchi zinaimarika kwa kuwa na afya bora, ili waweze kufanya vizuri shughuli zao za maendeleo.

Nae Mkurugenzi wa Bohari kuu ya Dawa Zahrani Ali Hamad,  amelishukuru shirika hilo na kuahidi kuyafanyia kazi maagizo yaliyotolewa na kuhakikisha dawa hizo zinatolewa kwa mujibu wa utaratibu.

Loading