WIZARA YA AFYA YAWATAKA WANANACHI KUPAMBANA NA MALARIA

Mkuu wa Kitengo cha Malaria Zanzibar Abdalla Suleiman akitoa maelezo kwa waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu kuwashajihisha Wananchi kusafisha mazingira yaliyowazunguka ili kupambana na Malaria huko Afisini kwake Mwanakwerekwe Wilaya ya Magharibi “B”.

MKUU wa Kitengo cha Malaria  Zanzibar Abdalla Suleiman amewataka wananchi kusafisha mazingira yao yanayowazunguka ili kupambana na maradhi ya malaria ambayo yameonyesha kujitokeza kwa wingi katika wilaya ya Magharibi  A na B pamoja na Wilaya ya kati kwa Unguja na baadhi ya  wilaya za Pemba  .

 Hayo aliyasema huko Ofisi kwake huko Mwanakwerekwe Wilaya ya Magharibi B wakati alipozungumza na waandishi wa habari Kwa lengo la kuwashajihisha jamii jinsi ya kupambana na malaria baada ya kuonekana yanaenea kwa kasi katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba .

Alisema takwimu zimeweza kuonyesha kuwa kwa upande wa kisiwa cha Pemba sehemu ambazo zimeweza kujitokeza wagonjwa wa malaria ni Micheweni ,Wete Tumbe pamoja na Wesha na kwa Unguja ni Shakani, Pangawe Fuoni Kibondeni,Cheju, Tunduni na Ndijani .

Aidha alisema maradhi ya malaria hujitokeza mara tu ya kumaliza mvua za masika kutokana na vindimbwi vingi vya maji vilivyotuwama  na kusabisha mazalio ya mbu hao pia kuna baadhi ya wagonjwa ambao wamejitokeza katika wilaya ya mjini wameonekana kutokea nje ya Zanzibar .

Alifahamisha kuwa malaria yaliopo kwa sasa sio ya kutisha lakini aliwataka wananchi kujitahidi kuweka mazingira safi ili kuweza kuyatokomeza mazalio ambayo ni chanzo cha maradhi kama vile mabupuru ya madafu ,maji machafu yaliotuwama katika maeneo mbali mbali .

Aliitaka jamii kujikinga kwa kutumia nguo ambazo zitaziba mbu wasiweze kushambulia mwili hasa wakiwa nje ya nyumba zao kama vile wakitizama televisheni nje ya maeneo ya nyumba zao

“Wananchi wanaokaa njeya nyumba zao kwa  muda mrefu hasa wakati wa usiku wametakiwa kutumie nguo zenye mikono mirefu na suruwali refu pamoja na soksi ili kuweza kuwadhibiti mbu wasiweze kuwashambulia .”alisema Mkuu huyo .

Hata hivyo aliwataka wananchi kufika katika vituo vya afya pale tu wanapojibaini wana maumivu ili kuweza kufanyiwa vipimo na kutoa ushirikiano na maofisa wa afya pindipo akibainika ana homa ya malaria ili kuweza kufanyiwa uchunguzi kwa wakaazi wanaoishi katika nyumba ambayo anatoka mgonjwa huyo.

Nae Afisa Muhamasishaji wa kitengo cha malaria Mwinyi Issa Khamis amewataka mama wajawazito na wenye watoto wadogo  kudai chandaruwa  wakati anapohudhuria kituo cha afya  na wananchi ambao wanamahitaji maalum kufika kwa sheha kuchukua kadi ya kitambulisho ili kupata chandarua .

Hata hivyo aliwataka wananchi wawe makini wanapotaka kuvitumia  vyandarua hivyowakati wanapotaka kuvitumia  kuvitoa ndani ya mfuko na kuviweka kwa muda wa masaa 24 au kuvifua kabla ya kuvitumia kwa sabuni bila ya kuvianika juani

Aidha alisema vyandarua hivyo havina sumu kwa binaadamu isipokuwa vimewekwa  dawa ya  kuulia mbu tu,iwapo binaadamu akitumia bila ya kufuata  maelekezo ya waataalamu watapata muwasho kidogo kutokana na dawa iliyowekwa .

Loading