ZANZIBAR YAZINDUA MKAKATI WA AFYA YA JAMII

Waziri wa Biashara na Viwanda Balozi Amina Salum Ali akifungua Mkutano wa 12 wa sekta ya afya unaofanyika Hoteli ya Verde Mtoni, Mjini Zanzibar.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imezindua mkakati wa Afya ya Jamii wenye lengo la kuhakikisha huduma za Afya zinaimarika zaidi kuanzia ngazi ya familia.

Mkakati huo umezinduliwa na Waziri wa Biashara na Viwanda Balozi Amina Salum Ali katika mkutano wa 12 wa kutathmini shughuli za sekta ya Afya Zanzibar unaofanyika Hoteli ya Verde Mtoni.

Waziri Amina alisema Zanzibar imepiga hatua kubwa katika kusambaza huduma za Afya Mijini na Vijijini lakini kuzinduliwa kwa Mkakati huo utapunguza changamoto zilizojitokeza miaka iliyopita na kuongeza ufanisi.

Alisema Serikali itafanya kila juhudi kuhakikisha Mkakati huo utakuwa endelevu kwani unagusa nyanja mbali mbali ikiwemo kupunguza vifo vya mama wajawazito wakati wa kujifungua na watoto wachanga.

Aliwataka wafanyakazi watakaoshughulikia Mkakati huo kuhakikisha wanatumia nafasi hiyo kuona malengo yaliyowekwa yanafikiwa.

Balozi Amina aliwashukuru washirika wa Maendeleo kwa michango yao mikubwa wanayotoa katika kuimarisha sekta ya Afya ambayo imeiwezesha Serikali kupiga hatua kubwa kusambaza huduma za Afya kwa wananchi.

Akizungumzia mafanikio yaliyofijkiwa katika sekta ya Afya, Katibu Mkuu Wizara hiyo Bi. Asha Abdalla alisema hatua kubwa imefikiwa katika kuimarisha Hospitali ya Mnazimmoja kufikia kuwa ya rufaa na moja ya Hospitali zinazotoa mafunzo katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Alisema Serikali imefanya juhudi kubwa kuongeza madaktari bingwa na wafanyakazi wa kada nyengine za afya na kuongeza vitendea kazi muhimu katika hospitali na vituo vya afya ambavyo vimeongeza ufanisi wa kutoa huduma.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya Zanzibar Asha Ali Abdalla akitoa hutuba katika Mkutano wa 12 wa kila mwaka wa kutathmini huduma za sekta ya Afya unaofanyika Hotel ya Verde Mtoni, Mjini Zanzibar.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya aliongeza kuwa hatua zilizochukuliwa na Serikali pamoja na wananchi kwa kushirikiana na washirika wa maendeleo Zanzibar imeweza kudhibiti maradhi ya Malaria ambayo yalikuwa yakiwasumbua wananchi wengi na kuathiri nguvu kazi ya kuimarisha uchumi.

Aidha alisema juhudi pia imechukuliwa kudhibiti kuenea kwa virusi vya HIV na kupunguza vifo vya akinamama vinavyotokana na uzazi wakati wa kujifungua.

Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Dk. Andemichael Ghirmay akizungumza na wadau mbalimbali wa sekta ya Afya Zanzibar katika Mkutano wa tathmini ya sekta ya afya unaofanyika Hoteli ya Verde Mtoni, Mjini Zanzibar.

Mwakilishi wa Shirikiala la Afya Duniani (WHO) Zanzibar Dk. Ghirmay Andemichael aliipongeza Serikali kwa kufanikiwa kudhibiti maradhi ya malaria na kutokomeza maradhi ya kipindupindu ambayo miaka michache iliyopita ilikuwa tishio kwa wananchi.

Alisema uwamuzi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuongeza bajeti ya Wizara ya Afya kila mwaka imeleta mafanikio makubwa katika kuwapatia huduma wananchi.

Dkt. Ghirmay alisema Washirika wa Maendeleo wataendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha huduma mbali mbali za jamii ikiwemo huduma katika sekta ya Afya.

Mkutano huo wa siku mbili unawashirikisha maafisa kutoka Wizara ya Afya Unguja na Pemba, Taasisi za kiraia na washirika wa Maendeleo kutoka Mashirika ya kimataifa.

Loading